MKOA WA RUKWA WAJIVUNIA MAFANIKO KATIKA TASNIA YA UTOAJI WA HAKI

 Na Mwandishi Maalum

Mkoa wa Rukwa  umeeleza mafanikio  chanya  katika  Utoaji Haki, mafaniko ambayo yamewafanya wananchi wa mkoa huo  kuishi kwa amani na usalama na hivyo kuweka mazingira rafiki kwa maendeleo ya Mkoa na Taifa kwa ujumla.

Hayo yamo katika taarifa fupi ya Mkoa huo  kuhusu hali ya utekelezaji wa Hakijinai taarifa ambao imeainisha mafanikio na changamoto.

 Taarifa hiyo ilisomwa na Wakili Frida  Hava  wakati wa kikao kati ya Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria, Profesa Sifuni Mchome, Dkt. Laurean Ndumbalo Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Dkt. John Jingu Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na Wadau wa Hakijinai Mkoa wa Rukwa.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo mafanikio hayo yamechangiwa  pamoja na mambo mengine na uwepo wa , na ushirikiano wa Idara ,Ofisi na  Taasisi mbalimbali zinazoisaidia  Mahakama katika kutenda haki.

Baadhi ya Ofisi   hizo ni kuanzishwa kwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali  na Huduma kwa Jamii na Sheria ya Majaribio na Ujenzi wa Tabia.

“Uwepo wa vyombo hivyo na vingine katika mkoa wetu umeleta mafaniko chanya ambayo yametokana na  utendaji   kazi wake. Utoaji haki unawafanya Wananchi wa Mkoa wa Rukwa kuishi kwa amani na usalama  hivyo kuweka mazingira rafiki kwa maendeleo ya Mkoa na nchi kwa ujumla” inasomeka taarifa hiyo.

Taarifa hiyo pia imeeleza kwamba, malalamiko mengi ya wananchi yamekuwa yakishughulikiwa na vyombo hivyo vya utoaji haki kwa weledi na ufanisi mkubwa  na hivyo kupunguza malalamiko kutoka  kwa wananchi ambayo yangefikishwa katika Ofisi za Serikali na  kushughulikiwa pasipo kufuata misingi ya utoaji wa haki.

Aidha Mkoa wa Rukwa unajivunia kuendelea  kupungua  kwa msongamano wa wafungwa gerezani hasa baada ya kuanzishwaji wa Huduma kwa Jamii na Sheria ya Majaribio ya Ujenzi wa Tabia mwaka 2018 ambapo hadi sasa mkoa una wataalamu wawili wanaoshughulika na  utoaji wa huduma hiyo.

“Kwa rejea, tangu mwezi Agosti, 2018  hadi Mei, 2021 Idara ya Huduma za Uangalizi imefanikiwa kutoa jumla ya  wafungwa wa kifungo cha nje 136. Kwa kuwa Idara  hii inahamasisha utoaji wa Adhabu  Mbadala imesaidia kupunguza gharama kwa Serikali katika kuwahudumia wafungwa na kuwasaidia wahalifu wadogo wasiende kujifunza mbinu mpya za uhalifu pindi wanapokuwa gerezani”.Inasema taarifa.

Pamoja na mafakio hayo , Mkoa wa Rukwa na kwa mujibu wa taarifa hiyo,  unakabiliwa na  changamoto kadhaa katika utekelezaji wa Hakijinai.

Baadhi ya changamoto hizo ni pamoja na, kwa  baadhi ya vyombo vinavyohusika kutoa haki kulalamikiwa kujihusisha na rushwa na kusababisha  haki ya wananchi kupotea kabisa au kuchelewa kabisa.

Changamoto nyingine ni kwa baadhi ya vyombo vya utoaji haki  kuingiliwa na vyombo vingine visivyo na mamlaka ya kutoa haki mfano Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) huingiliwa utendaji wake na watendaji wa  Serikali.

Changamoto nyingine ni kwa baadhi ya watuhumiwa  kulalamikia kitendo cha kubambikiziwa kesi na  walalamikaji kwa kushirikiana na  Idara za kutoa haki ambazo hazina uaminifu kwa lengo la kuwakomoa au kulipa kisasi.

Kutofikishwa mahakamani kwa kesi nyingi za  mahabusi kwa kigezo cha upelelezi kutokamilika kunawafanya mahabusu hao kukaa muda mrefu gerezani na kuisababisha Serikali hasara na kuchelewesha haki kwa mahabusu hao ni moja ya changamoto inayoukabili  Mkoa huo katika uotaji ya Hakijinai

Changamoto nyingine ni wafungwa wengi kushindwa kukata rufaa kutokana na kukosa nakala za hukumu au nakala za  hukumu kucheleweshwa sana kutolewa, hali hii imepelekea wafungwa wengine kumaliza kifungo bila kutekeleza haki yao ya kukata rufaa.

Mkoa huo wa Rukwa pia unakabiliwa na changamoto ya kukosekana kwa wakalimani wakati wa kusikiliza kesi au malalamiko yao hasa wa lugha adimu  za kigeni  wakitolea mfano lugha ya kichina na lugha ya alama kwa watu wenye ulemavu.

Changamoto ya kukosekana kwa wakalimani wa lugha za kigeni  na alama kumeelezwa kukwamisha chombo kinachohusika na  mwenendo wa shauri fulani kushindwa kuendelea hadi hapo mkalimani atakapopatikana.

Mwamko hafifu wa Wananchi katika kutoa ushirikiano kwa wahanga wa matukio ya uhalifu hasa yanayohusu maadili kama  mimba za utotoni, ubakaji, ulawiti, ndoa za utotoni na udhalilishaji.

 Akijibu baadhi ya changamoto hizo, ikiwamo ya baadhi   vyombo vya  utoaji haki kuingiliwa na vyombo visivyo na mamlaka ya  utoaji haki, Katibu Mkuu  Katiba na Sheria, Profesa Sifuni Mchome ametaka jambo hili liachwe mara moja   na  kila chombo  kitekeleze majukumu yake  bila kuingilia chombo kingine.

Amewasisitiza  watumishi kutekeleza  majukumu yao kwa kuzingatia weledi, maadili na miongozo ya utumishi wa umma na kamwe wasipindishe sheria.

Kuhusu baadhi ya  watendaji katika vyombo  vya utoaji wahaki  kulalamikiwa kuchukua rushwa, Profesa Mchome ameitaka TAKUKURU kutimiza wajibu wake.

Imetolewa na Maura Mwingira


Mrakibu wa Magereza Mkoani Rukwa  SP Daniel Ndamgilire akichangia majadiliano kuhusu hali ya utoaji haki ilivyo katika Mkoa wa Rukwa


Makatibu Wakuu, Katiba na Sheria, Utumishi na Maendeleo ya Jamii, JInsia, Wazee na Watoto wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi wa wadau wa vyombo vya Utoaji haki, mara tu baada ya kikao chao kilichofanyika siku ya Alhamisi ambao mafanikio na changamoto za utoaji haki katika mkoa huo zilijadiliwa. Makatibu Wakuu hao wapo katika ziara ya kikazi ya kawaida ya kutembelea Mikoa ya Songwe, Rukwa na Katavi

Leave a Comment

No comments: