MWAKYEMBE AMTAMBULISHA RASMI KAIMU KATIBU MTENDAJI WA BODI YA FILAMU.

* Dkt. Kiagho Kilonzo ahaidi kuleta mabadiliko na kuhakikisha 
Filamu inakuwa jukwaa rasmi la uchumi hapa nchini.

Na.Khadija seif,Globu ya jamii

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe  mapema leo amekutana na Bodi ya Ushauri ya Bodi ya Filamu nchini katika ofisi za  Bodi ya Filamu na kumtambulisha kwa Wajumbe wa Bodi hiyo Kaimu Katibu Mtendaji  mpya wa Bodi ya Filamu Tanzania Dkt. Kiagho Kilonzo.

Katika kikao hicho Mhe. Mwakyembe alipongeza jitihada chanya zilizoanza kufanywa  na Naibu Katibu Mtendaji huyo katika kipindi kifupi cha kuteuliwa kwake na kumtaka  kufanya kazi kwa bidii na weledi wa hali ya juu katika kuhakikisha Sekta ya Filamu na  Michezo ya Kuigiza inasonga mbele na kuwa sehemu ya pato kwa Taifa na Wanatasnia 
wenyewe.

“Sekta ya Filamu na Michezo ya Kuigiza ni moja ya Sekta kubwa na muhimu 
zinazoweza kukuza pato la nchi na kupunguza umaskini kwa raia wake, hivyo Bodi ya  Filamu ni wajibu wenu kutengeneza mazingira rafiki yatakayo wezesha Sekta hii  kukuwa hapa nchini na kupunguza umaskini kwa Watendaji wake” Dkt. Mwakyembe  alisema.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mtendaji mpya wa Bodi ya Filamu Tanzania Dkt.  Kiagho Kilonzo alimshukuru Waziri Mwakyembe kwa kushiriki katika kikao hicho cha  kutambulishwa kwake kwa Wajumbe wa Bodi ya Ushauri ya Bodi ya Filamu  na kumuahidi kuendelea kufanya kazi nzuri itakayoimarisha na kukuza Tasnia ya  Filamu kwa kushirikiana na Wajumbe hao wa bodi ya Ushauri inayoongozwa na  Mwenyekiti wake Profesa Frowin Nyoni, kushirikiana na Wadau mbalimbali wa Sekta ya  Filamu na kuimarisha umoja wa vyama vya Watendaji katika Filamu ili kuhakikisha 
Filamu inakuwa jukwaa rasmi la uchumi hapa nchini.

“kwa pamoja tutashirikiana katika kuifanya Sekta ya Filamu na Michezo ya Kuigiza  inakuwa na mchango chanya kwa Taifa letu na sio sehemu au jukwaa la kuharibu  maadili ya kitanzania, hivyo tunaahidi kuifanya Sekta hii kuzidi kuimarika ili iweze kuwa  jukwaa la moja kwa moja la pato la mtu binafsi na Taifa kwa ujumla”. 

Hata hivyo bodi ya Ushauri ya Bodi ya Filamu kwa sasa ina wajumbe 8 ikiongozwa na Mwenyekiti Profesa. Frowin Nyoni na Katibu Dkt. Kiagho Kilonzo ambaye ni Naibu Katibu Mtendaji wa Bodi.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe  (katikati) akisisitiza jambo wakati wa Kikao cha kumtambulisha kwa Wajumbe wa Bodi  ya Ushauri ya Bodi ya Filamu Tanzania Kaimu Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu  Tanzania Dkt. Kiagho Kilonzo (kulia) katika Ukumbi wa mikutano wa Bodi hiyo iliyopo  Mtaa wa Samora Posta jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi hiyo 
Profesa Frowin Nyoni.

No comments: