SERIKALI YATOA FEDHA KUJENGA SHULE MPYA YA SEKONDARI KATA YA MSANJA, KILINDI.

Wananchi wa Jimbo la Kilindi wamepokea kwa furaha taarifa ya Serikali kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya sekondari katika Kata ya Msanja, Kijiji cha Muungano Jimbo la Kilindi, Hatua hiyo inalenga kuongeza fursa za elimu kwa vijana pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia katika eneo hilo.

Mradi huo unatarajiwa kuanza kutekelezwa mara moja na utasaidia kupunguza changamoto ya wanafunzi kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za elimu ya sekondari, hali itakayowezesha upatikanaji wa elimu kwa urahisi zaidi kwa wakazi wa Kata ya Msanja na maeneo jirani.

Akizungumza kuhusu maendeleo hayo, Juni 11, 2026, Mbunge wa Jimbo la Kilindi, Mhe. Salehe Mbwana Mhando, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu na kutekeleza miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Wananchi wa Kata ya Msanja na Jimbo la Kilindi kwa ujumla wameeleza shukrani zao kwa Serikali kwa kuendelea kuwaletea miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa jamii, aidha wameahidi kutoa ushirikiano unaohitajika ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyostahili.



No comments: