ONGEZENI KASI YA KUFANYA MIKUSANYO YA MAKUMBUSHO IZUNGUMZE NA JAMII: DKT LWOGA

 

Na Sixmund J. Begashe

Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa Dkt Noel Lwoga, amewataka wataalam wa Taasisi hiyo kuongeza kasi ya kuhakikisha inaongeza kasi katika kuhakikisha jamii inakuwa karibu na Makumbusho zote nchini ili mikusanyo iliyopo iweze kutumiwa na jamii katika kujielimisha, kujikumbusha na kuburudika.

Dkt Lwoga ameyasema hayo kwenye kikao maalumu na wafanyakazi wa Taasisi hiyo kilichofanyika Makumbusho na Nyumba ya Utamaduni Dar es Salaam, chenye lengo la kuhakikisha wafanyakazi wote wanaelewa kuhusu Mpango Mkakati wa Taasisi wa Miaka Mitano 2021/2025.

Mmekuwa Mkifanya vizuri kwenye mambo mbalimbali hasa katika kubuni program na matamasha, lakini nawataka muongeze kasi katika kuhakikisha vituo vinakuwa na program nyingi zitakazo wavuta watu mbalimbali kuingia kwenye makumbusho zote, program hizo zitachochea mikusanyo yetu iwe karibu na jamii” Dkt Lwoga

Dkt Lwoga amesema Taasisi yake imejipanga vyema katika kuongeza idadi ya mikusanyo ya kimakumbusho pamoja na kuongeza idadi ya makumbusho na vituo vya utafiti ili kuboresha huduma kwa jamii.

Licha ya kuongeza idadi ya mikusanyo na kuanzisha makumbusho nyingine, taasisi inalengo la kuanzisha maonesho 12 ya kudumu, maonesho 8 ya muda, kuwa na matamasha 50, kuwa na mikataba ya kimataifa na yandani, kuwaendeleza wafanyakazi kielimu na kuboresha maslai ya watumishi” Aliongeza Dkt Lwoga

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu, Bibi Nuru Sovella alimpongeza Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa kwa kurithia vikao vya mara kwa mara vya wafanyakazi vyenye lengo la kutatua kero na kutoa maagizo kwa watumishi.

Akizungumzia mikakati ya Makumbusho ya Taifa, Afisa Mipango wa Taasisi, Felix Mukuku amesema kuwa Mpango Mkakati huo una lengo la kuipeleka Makumbusho ya Taifa mbele zaidi na kwamba una kazi 121 zinazotakiwa kutekelezwa kwa ufanisi mkubwa.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi (RAAWU) Bw. Anastasius Liwewa aliipongeza ofisi ya Mkurugenzi Mkuu kwa kupokea malalamiko ya wafanyaki na kuyafanyia kazi kwa haraka hasa katika kuboresha maslai ya wafanyakazi, hivyo amewaomba wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii, weledi na kasi zadi ili malengo ya taasisi yaweze kufanikiwa.

Katika kikao hicho watumishi walipewa elimu juu ya maambukizi ya ukimwi na Uviko 19 yaliyotolewa na wataalamu kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.


 

No comments: