DAWASA yapeleka neema Madale, Mivumoni, Kulangwa na Nakasangwe

 

MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), imemaliza tatizo la maji kwa wananchi wa Madale, Mivumoni, Kulangwa na Nakasangwe, baada ya kufunga pampu mpya ya kusukuma maji eneo la El-maary Madale.

Maeneo hayo, yalilazimika kupata huduma ya majisafi kwa mgao au yakitoka machache kutokana na msukumo kuwa mdogo, hivyo kuwafanya wananchi wa maeneo hayo kusotea huduma hiyo.

Kukamilika kwa ujenzi wa pampu hiyo ya kusukuma maji iliyoanza kujengwa 12 Desemba 2020, kumekuwa faraja kwa wakazi hao ambao wamesema, kwa sasa shughuli zao zitakwenda sawia.

Meneja wa mkoa wa kihuduma DAWASA Mivumoni, Mhandisi Felchesm Kimaro amesema, maeneo ya Kwa mpetapae, Maigwaigwa, Lemoni, Flamingo, Kwa Ngamange, Mother of mess, Kwa kawawa, Sheraton na Mkoroshini watakua wanufaika wa pampu hiyo ambayo inahudumia zaidi ya wakazi 600.

“Uwepo wa pampu hii, utasaidia upatikanaji wa maji wa uhakika ndani ya wiki nzima na kupunguza mgao wa maji kwa kiasi kikubwa katika baadhi ya maeneo," amesema Mhandisi Kimaro
"Pia, kwa upande wa DAWASA, faida kubwa itakayopata ni ongezeko la makusanyo kwani sasa idadi ya wateja watakao kua wanapata huduma itaongezeaka na mgao utakwisha," amesema 

Kwa upande wao, wananchi nao hawakusita kuonyesha furaha yao juu ya kumalizika kwa ujenzi wa pampu hiyo kwani imekuwa msaada mkubwa kwao kupambana na adha ya maji.

“Tunaishukuru DAWASA kwakutujengea pampu hii ambayo sasa inamaliza changamoto zetu za huduma ya maji. Tulikuwa tunakaa muda ndani ya wiki bila upatikanaji wa maji, kitu ambacho kilikwamisha sana shughuli zetu za maendeleo," amesema Datus Peter

Amesema kwa sasa shughuli zao zitakwenda vizuri bila tatizo lolote.

Lengo la DAWASA kwa sasa ni kuzifikia sehemu zote ambazo huduma ya maji haijafika ili kuwasogezea wananchi huduma hiyo muhimu karibu zaidi.

No comments: