KIBAHA MJI,MKURANGA NA CHALINZE ZAONGOZA MAAMBUKIZI MAPYA PWANI-NDIKILO





……………………………………………………………………………
NA MWAMVUA MWINYI,PWANI 


MKUU wa Mkoa wa Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo ametaja Halmashauri ya Kibaha Mji, Mkuranga na Chalinze kuwa na maambukizi mengi ukilinganisha na halmashauri nyingine mkoani humo, kutokana na uwepo wa shughuli nyingi za mwingiliano wa kiuchumi. 


Kutokana na hali hiyo ,amewataka Viongozi na Wadau mbalimbali Mkoani hapo, kuweka mikakati madhubuti kupambana na kushusha maambukizi mapya ya VVU.
Aliyaweka bayana hayo,wakati wa maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani yalifanyika kimkoa Wilayani Bagamoyo katika Viwanja vya Shule ya Msingi Majengo. 


Akizungumza na Wananchi ,Ndikilo alisema Takwimu zinaonesha kiwango cha maambukizi Kimkoa Kimepungua kutoka asilimia 5.9 mwaka 2012 hadi asilimia 5.5 mwaka 2017, ..ingawa bado yapo juu ya Wastani wa kitaifa ukilinganishe na kile cha Taifa cha asilimia 4.7. 


Alitaja Changamoto zinazochochea mapambano dhidi ya VVU Mkoani hapo kuwa ni Ndoa za utotoni, kuwepo kwa vituo vya maegesho ya malori kwenye barabara kuu, ulevi uliopindukia, ngoma za usiku (Vigodoro), kuwepo kwa biashara ya Ngono, ikiwemo vigodoro. 


Aidha mkuu huyo wa mkoa, aliwaasa wanaume kuacha uoga wa kupima VVU kwani idadi ya wanawake wanaonekana kupima kuliko wanaume. Ndikilo aliwataka Waishio na Virusi vya UKIMWI wasibweteke na kufubazwa kwa VVU na kuanza mienendo isiyofaa. 


Ndikilo alitoa rai, kwa wadau mbalimbali wanaoshughulika na Masuala ya Udhibiti wa UKIMWI kuendeleza mapambano, ikiwemo Halmashauri kuwa na Sheria ndogo za kudhibiti sherehe na shughuli mbalimbali zenye viashiria vya UKIMWI.

No comments: