BONDE LA WAMI/RUVU KUFUNGA MITA ZA MAJI KWA WENYE VIWANDA

  

Afisa Maji wa Bondel la Wami/Ruvu Mhandisi Simon Ngonyani akizungumza na waandishi Habari kuhusiana na masuala mbalimbali ya bonde hilo leo jijini Dar es Salaam.

*Mhandisi Ngonyani awapongeza CTI katika utekelezaji wa sheria

Na Chalila Kibuda,Michuzi TV.

BODI ya Bonde la Wami-Ruvu wataendelea na zoezi la utambuzi wa watumiaji wa maji kwa kuwasajili ili ifikapo Februari 2021 ili waweze kuwa na namba ya uhakika ya watumiaji wa maji hapa nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam, Afisa Maji wa bodi hiyo Mhandisi Simon Ngonyani amesema katika kuendelea kulinda rasilimali za maji bonde la Wami-Ruvu wamekubaliana na wadau  wenye Viwanda (CTI,) makampuni na taasisi mbalimbali kufunga mita ili kupata kiwango sahihi cha maji wanachotumia.

Mhandisi Ngonyani amesema kuwa vyanzo vya maji lazima vitunzwe na fedha zinazokusanywa zinatakiwa kutumika katika vyanzo hivyo.

"Watu wamekuwa wakiona maji wanatambua mamlaka bila kutambua maji hayo kuna watu ndio wanalinda vyanzo hivyo." amesema Ngonyani.

"Zoezi hili litaanza kwa wadau wenye viwanda, hii yote ni katika kujua matumizi halisi ya maji hapa nchini yalivyo ili itusaidie kupanga mipango ya watumia maji vizuri." Amesema Ngonyani.

Aidha Ngonyani amesema mabadiliko ya tabia nchi yanapelekea vyanzo vya maji kuwa hatarini kupungua uwezo wake kwa kiasi kikubwa.

Hata hivyo amesema wamekuwa wakilazimika kuleta mbadala wa shughuli za kibinadamu ambazo haziathiri vyanzo vya maji kama upandaji wa miti ya matunda kwenye vyanzo vya maji.

Pamoja na hayo amewataka watumiaji wa visima vya maji vya kibiashara na sio matumizi ya nyumbani kulipa ada zao kulingana na matumizi (kwa wenye vibali) na wasio na vibali wanatakiwa kufika ofisini kwa ajili ya kupata utaratibu wa kupata vibali.

No comments: